JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

SHIRIKA LA POSTA TANZANIA

Habari

MKAPA AHIMIZA TEKNOLOJIA POSTA


Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Bw. Nicholaus Merinyo Mkapa, amehimiza ubunifu na teknolojia katika huduma za Posta kama sehemu ya kuadhimisha Siku ya Posta Duniani ambapo maadhimisho haya yanakumbusha mchango mkubwa wa sekta ya Posta katika maendeleo ya kiuchumi, kijamii na kiteknolojia duniani.

Akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Posta Duniani yaliyofanyika leo tarehe 09 oktoba, 2025 katika ukumbi wa Tanzanite, Millenium Tower jijini Dar es Salaam, Bw. Mkapa alisema kuwa kaulimbiu ya mwaka huu, “Posta kwa Ajili ya Watu: Huduma za Kizawa. Ufikaji  Kimataifa.” inakumbusha dhamira ya sekta ya Posta kama injini ya maendeleo endelevu kupitia matumizi ya TEHAMA, utoaji wa huduma jumuishi, na ushirikishwaji wa vijana katika ubunifu na ujasiriamali.

Naibu Katibu Mkuu ameeleza kuwa Kaulimbiu hii inatukumbusha wajibu wa Posta kuwafikia wananchi popote walipo na kuwaunganisha na fursa za kimataifa na imekuwa fahari kuona Shirika la Posta na wadau wake wamepokea mabadiliko ya kiteknolojia kwa mtazamo chanya, wakihakikisha wananchi wananufaika na huduma hizo.

Aidha, Bw. Mkapa amesema Wizara imeendelea kuwezesha sekta ya Posta nchini kwa kuweka sera bora na kanuni zinazowezesha utoaji wa huduma bora na upanuzi wa sekta ya TEHAMA, ili kuiwezesha Tanzania kuelekea uchumi wa kidigitali.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Dkt. Jabiri Kuwe Bakari, alisema kuwa sekta ya Posta ni muhimili muhimu katika uchumi wa kidijitali, kwani kila usafirishaji na ununuzi mtandaoni unategemea mfumo wa Posta kwani asilimia kubwa ya biashara mtandaoni inahitaji mifumo ya usafirishaji inaoaminika hasa ya Posta na huo ndio msingi wa Posta.

Naye Mkurugenzi wa Huduma za Posta Bw. Arubee Ngaruka akiongea kwa niaba ya Postamasta Mkuu wa Shirika la Posta Tanzania, Bw. Macrice Mbodo alisisitiza kuwa Shirika linaendelea kubadilika na kuwekeza katika teknolojia za kisasa ili kuhakikisha huduma za Posta zinafika kwa wananchi wote, ikiwemo maeneo ya vijijini ambako watoa huduma wengine hawafiki.

Maadhimisho ya mwaka huu yamehudhuriwa na viongozi mbalimbali kutoka serikalini, taasisi za mawasiliano, wanafunzi, walimu na wadau wa sekta ya posta, yakisisitiza dhamira ya Shirika la Posta Tanzania kuendelea kuwa kiunganishi cha wananchi na dunia kupitia huduma za kisasa, salama na jumuishi.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano
Shirika la Posta Tanzania


© SHIRIKA LA POSTA TANZANIA