Habari
WAFANYAKAZI WAASWA KUONGEZA BIDII

Mkurugenzi wa Rasilimali watu Bw. Amwesiga Kamihanda kwa niaba ya Postamasta Mkuu Bw. Macrice Mbodo amewaasa wafanyakazi wa Shirika la Posta Tanzania kuongeza bidii ili kuyaishi malengo ya Shirika na kuendelea kutoa huduma bora kulingana na mahitaji ya sasa ya wananchi na kuleta tija kwa Taifa. Ameyasema hayo tarehe 01 Mei, 2025 katika Hoteli ya KBH iliyopo Singida, wakati wa Hafla fupi ya kumpongeza mfanyakazi Hodari Kitaifa. Wakati wa Hafla hiyo, Bw. Kamihanda alieleza kuwa katika maendeleo ya teknolojia yanayoendelea kwa kasi duniani Posta haina budi kujipanga upya kila wakati ili kuhakikisha linaendelea kuwa la kisasa, shindani na la kuaminika. Aidha, Bw. Kamihanda alitumia nafasi hiyo kumpongeza mfanyakazi Hodari Kitaifa Bi. Frida Masoy ambaye ni mfanyakazi wa Posta Mkoa wa Arusha na kueleza kuwa Shirika linatambua kazi nzuri anayofanya, na kuwa mfano huu utaamsha ari mpya kwa wafanyakazi wengine katika kulitumikia Shirika. Imetolewa na; Kitengo cha Mawasiliano; Shirika la Posta Tanzania.